Mbele ya makada kadhaa na wabunge pamoja na maseneta kutoka chama tawala waliokutana katika mkutano wa chama mjini Abidjan Jumatano wiki hii kuomba akubali kuwania katika uchaguzi wa urais kwa muhula wa tatu, rais Alassane Ouattara amejizuia kutoa uamuzi wake.
Rais Ouattara alitangaza baada ya mkutano wa chama chake cha RHDP kuwa;"Kwa huzuni na mapenzi niliyokuwa nayo kwa Amadou, kwa mwanangu, ninazingatia maazimio ya baraza la kisiasa na ombi lake, Ninawaomba muendelee kumuenzi Amadou Gon Coulibaly na mnipe muda wa kupumzika na kutafakari, kabla ya kuwapa jibu haraka iwezekanavyo "
Rais wa Côte d'Ivoire alielezea wazi kuwa atalihutubia taifa hivi karibuni, na akasisitiza matakwa yake kuona chama cha RHDP kinashinda uchaguzi.
"Tunapaswa kujivunia kile tumeshafanya na ndiyo sababu lazima tuendee na njia hiyo. Nitatoa jibu langu hivi karibuni, na nitalihutubia taifa kusema kile ambacho ni changamoto kwa nchi yetu, kwa nini Côte d'Ivoire inatakiwa kuendelee kama hii leo. Nchi hiii haitakiwi kuwa mikononi mwa watu ambao wanaweza kuhatarisha usalama wa taifa na kutete amaslahi yao, "amebaini rais Alassane Ouattara.
Tangu kifo cha Waziri Mkuu Amadou Gon Coulibaly mapema mwezi Julai, wajumbe mbalimbali kutoka chama cha RHDP wamekuwa wakimshinikiza rais Ouattara kuwania katika uchaguzi wa urais wa mwezi Oktoba.
Wiki iliyopita, kwa ombi la Mkurugenzi Mtendaji wa chama tawala, Adamu Bictogo, wabunge na Maseneta kutoka chama hicho, walikutana huko Abidjan, na kila mmoja aliomba Rais Ouattara kuwania kwenye kiti cha urais katika uchaguzi wa urais.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Waziri wa Ulinzi na Kaimu Waziri Mkuu Hamed Bakayoko alitoa wito kwa rais Outtara kuwania kwenye kiti cha urais katika uchaguzi ujao.