Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA John Mnyika amelitaka Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina na kuwabaini waliomvamia, kumpiga na kumjeruhi mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe akiwa nyumbani kwake Area D Jijini Dodoma.
Katibu Mkuu huyo amesema kuwa; "Waliomshambulia Mwenyekiti Freeman Mbowe wakati wakitekeleza tukio hilo la kikatili walikuwa wakitamka maneno wakisema kuwa 'wewe unaisumbua sana Serikali, na tuone sasa kama utaweza kufanya kampeni. Kutokana na kauli hii, tumeshangazwa na hatua ya jeshi la Polisi kujitokeza mapema kabisa na kueleza kuwa tukio hilo
halifungamani na masuala ya kisiasa kabla ya kuanza kufanya uchunguzi".
Pia Mnyika amesema "tunalitaka Jeshi la Polisi kumhoji Mchungaji Mashimo ambaye siku za karibuni alitamka kuwa kuna kiongozi mkubwa wa chama cha siasa siku si nyingi atapigwa na kujeruhiwa, kama chama baada ya tukio la kushambuliwa kwa mwenyekiti wetu Freeman Mbowe usiku wa kuamkia leo, tunaona huenda mchungaji huyo anafahamu wahusika wa tukio hili".
Freeman Mbowe ameshambuliwa na watu wasiojulikana usiku wa kuamkia leo jumanne na kwasasa amelazwa katika hospitali ya Ntyuka Mjini Dodoma, Na tayari Chama hicho kinaandaa utaratibu wa kumsafirisha kwenda Jijini Dar es salaam kwa ajili ya matibabu zaidi.