Ikiwa leo ni siku ya Wakunga Duniani, Chama cha wakunga Tanzania (TAMA) kimewashauri wakunga wote kuvaa vifaa muhimu vilivyotakaswa hususani wakati huu wa COVID-19 ili kumlinda mama na mtoto dhidi ya maambukizi ya ugonjwa huo.
Hayo yamebainishwa na Katibu wa Chama cha Wakunga Tanzania Dkt. Sebalda Reshabari wakati akihojiwa katika kipindi cha Tuongee Asubuhi kinachorushwa na StarTv.
Kwa upande wake Hilda Mushi ambaye ni Mkunga Mwandamizi kutoka hospitali ya Mount Meru iliyoko Arusha amesema matamanio yake ni kuona vifo vitokanavyo na watoto wachanga na akina mama vinapungua.
Hivyo kwa wakati huu ambao janga la Corona linaendelea kuitikisa Dunia amewasihi mama wajawazito na ambao wameshajifungua kutosita kuwatumia Wakunga wanaowahudumia hususani kwa kuwapa elimu ya kumlea mtoto vyema dhidi ya kuepuka maambukizi ya Corona.
Baadhi ya Wakunga hawakusita kuzungumzia juu ya lugha zisizo rafiki kwao ambazo wanakutana nazo mahala pa kazi zikiwemo za kejeli na matusi kutoka kwa mama wajawazito pamoja na ndugu zao wanaokwenda kujifungua.
Mwaka huu wa 2020 umetangazwa na Umoja wa Mataifa kuwa mwaka wa wauguzi na wakunga ili kutambua mchango wa wahudumu hao wa sekta ya afya.