Wakati Dunia ikipambana na kukabiliana na kuenea kwa virusi vya Corona kwa kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuzuia mikusanyiko kwa kufunga shule na baadhi ya Taasisi, Wazazi na Walezi mkoani Njombe wamelalamikiwa kwa madai ya kuwatumikisha watoto katika kipindi hiki ambacho shule zimefungwa.
Kufungwa kwa shule na baadhi ya Taasisi mbalimbali zinazoendeshwa kwa mikusanyiko ni njia mojawapo ambayo inatumika na nchi mbalimbali ulimwenguni kote ikiwa ni kukabiliana na kuenea kwa virusi vya korona.
Wazazi hao wameelezwa kuwatumikisha wanafunzi hao ambao ni watoto wao kwa kuwapa kazi ya kwenda kuuza bidhaa sokoni badala ya kuwaacha wakae nyumbani kwa kujisomea kipindi hiki ambacho shule zimefungwa kwasababu ya ugonjwa wa Corona.
Kwasasa baadhi ya maeneo nchini Tanzania yamekuwa kama fursa kwa wazazi kuwatumia watoto wa shule kufanya biashara na kuendesha shughuli mbalimbali za nyumbani tofauti na mtazamo wa serikali ulivyokuwa.
Mfumo uliopo kwa sasa kipindi hiki ambacho wanafunzi hawaendi shule nchini Tanzania, wanasoma kupitia vituo vya radio na televisheni na vilevile mitandao ya kijamii ikiwemo WhatsApp.
Mtizamo wa baadhi ya wazazi kuhusu mfumo huu, wanaona unawapa wakati mgumu wanafunzi na wanadhani kwamba huenda kusiwe na matokeo mazuri katika mitihani yao ya mwisho kwa Watoto wao kutokuwa na uwezo wakufuatilia masomo hayo kwa njia ya mtandao.
Baadhi ya wazazi wamesema kuna haja ya ufuatiliaji wa karibu juu ya watoto wao kuweza kufanyika ili kuwafanya wanafunzi wawe huru kwa kupata muda wa kujisomea wakati huu ambao serikali inatafuta mbinu mbadala ya kukabiliana maambukizi ya virusi vya corona.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Afya nchini Tanzania siku ya Jumatano Aprili 29, 2020 ilieleza kuwa watu 167 waliopona maambukizi ya corona, visa 480 vya wagonjwa walioambukizwa virusi vya Corona na vifo vya watu kumi na sita.