Mwili wa aliyekuwa Askofu wa Kanisa la Mlima wa Moto (Mikocheni B, Assemblies of God) Dkt. Getrude Rwakatare tayari umepumzishwa katika nyumba ya milele ndani ya viunga vya kanisa hilo jijini Dar es Salaam.
Mazishi hayo yamefanyika leo Alhamisi Aprili 23, 2020, majira ya saa 7:00 mchana na kuhudhuriwa na watu wachache wa familia yake, lengo la watu hao wachache wa familia kuhudhuria likiwa ni kuepuka mikusanyiko kama tahadhari ya maambukizi ya Virusi vya Corona.
Taarifa za Mama Rwakatare kufariki Dunia zilitolewa Aprili 20,2020 na mwanaye Mutta Rwakatare.
Umauti ulimkuta Mama Rwakatare katika hospitali ya Rabininsia, alikokuwa akipatiwa matibabu, ambapo kwa mujibu wa mwanaye Mutta alisema kuwa Mama yake alikuwa akisumbuliwa na tatizo la moyo na presha.