Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na viongozi wa Dini Nchini imeandaa maombi maalum Kitaifa kuiombea Nchi dhidi ya maambukizi ya Virusi vya Corona.
Maombi hayo yataongozwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa viongozi wakuu wa madhehebu ya Dini nchini yatafanyika kesho Aprili 22,2020 Jumatano katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam kuanzia saa tatu kamili asubuhi.
Wizara imeeleza kuwa viongozi wachache watahudhuria maombi hayo kuwawakilisha wanachi ikiwa ni katika hali ya kuchukua tahadhari ya ugonjwa huo huku wananchi wakisisitizwa kufuatilia maombi kupitia vyombo vya habari.
Maombi hayo ni utekelezaji wa maazimio ya mkutano wa viongozi wa dini na serikali uliofanyika Aprili 9 mwaka huu, na pia ni mwendelezo wa siku tatu za maombi zlizotangazwa na Rais John Magufuli kuanzia Aprili 17-19, 2020.
Hapo Jana Aprili 21, Wizara ya Afya, ilitoa taarifa ya uwepo wa wagonjwa wapya 84 wa corona na kufanya visa vya corona kufikia 254 pamoja na vifo vipya vitatu vilivyotokea jijini Dar es Salaam vya watu waliothibitishwa kuwa na #COVID19.
Idadi hiyo ya vifo vipya vya watu watatu vilivyotangazwa jana vinafanya idadi ya waliofariki kwa corona nchini kufikia kumi.
Waziri wa Afya Ummy Mwalimu alisema wagonjwa hao wapya wamepatikana kuanzia Aprili 18 hadi Aprili 20 na kati yao, Wagonjwa 68 wamepatikana Tanzania Bara na 16 walipatikana Zanzibar.