Waziri wa afya Ummy Mwalimu ametoa taarifa ya uwepo wa ongezeko la wagonjwa wanne wa Corona ambapo watu hao wamepatikana Dar es Salaam, Mwanza , Kaskazini Magharibi mwa Tanzania na visiwani Zanzibar na kufikisha idadi watu 24 walio na maambukizi ugonjwa huo nchini.
Miongoni mwa wagonjwa hao wapya wa Tanzania bara ni mwanaume mwenye miaka 41 raia wa Tanzania, mfanyabiashara na mkazi wa Mwanza aliyeingia nchini humo akitokea Dubai tarehe 24 mwezi Machi kupitia uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere(JNIA) na kuelekea Mwanza tarehe 29 Machi.
Mgonjwa huyo alichukuliwa vipimo na kukutwa na virusi vya corona, na mgonjwa mwingine ni mwanaume mwenye miaka 35 raia wa Tanzania, mkazi wa Dar es Salaam ambaye pia ni mfanyabiashara.
Wagonjwa wawili ni wale walioripotiwa na Waziri wa afya wa Zanzibar tarehe 5 mwezi huu, mamlaka ya kisiwani Zanzibar ilitangaza siku ya Jumapili, Aprili 05 kuwa na maambukizi mapya ya watu wawili na hivyo kufanya kisiwa hicho kuwa na watu saba wenye maradhi ya corona.
Mgonjwa wa kwanza ana umri wa miaka 33, aliingia Zanzibar tarehe 18, Machi 2020 akiwa anatokea Tanga na mgonjwa wa pili ana miaka 27, alirejea kutoka mapumziko Tanga Machi 13, 2020.
Aidha Waziri Ummy amesema wagonjwa wote wako chini ya uangalizi wa watoa huduma za afya katika vituo maalumu vya tiba Dar es Salaam, Zanzibar na Mwanza.
Aprili Mosi, Wizara ya Afya nchini Tanzania ilitangaza ongezeko la mgonjwa mmoja wa virusi vya corona nchini na kufikisha idadi ya wagonjwa nchini humo kufikia 20.
Kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Afya Ummy Mwalimu, imeeleza kuwa mgonjwa huyo ni mwanamke mwenye miaka 42, raia wa Marekani alikuwa karibu na mtu aliyesafiri nje ya nchi na baadaye kuthibitika kuwa ana maambukizi ya virusi hivyo baada ya kurejea Tanzania.
Mwisho.