Watumishi watano wa Shirika la Reli Tanzania TRC wamefariki kwa ajali ya treni ya uokoaji iliyogongana na Kiberenge Na. HDT-3 katika eneo lililopo kati ya Stesheni ya Mwakinyumbi na Gendagenda katika reli inayotoka Ruvu Junction mpaka Mruanzi Junction, tarehe 22 Machi 2020.
Taarifa hiyo imetolewa leo katika vyombo vya habari na Jamila Mbarouk ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Habari na Uhusiano TRC imethibitisha kutokea kwa ajali hiyo ambayo imegharimu Maisha ya wafanyakazi wake watano.
Ajali hiyo imehusisha watumishi sita wa TRC ambapo watumishi wane walifariki eneo la ajali na majeruhi wawili walifikishwa katika Hospitali ya Wilaya ya (Magunga) iliyopo Korogwe mkoani Tanga kwa ajili ya huduma za kitabibu, ilipofikia saa tano usiku (23:00) tarehe 22 Machi 2020 majeruhi mmoja alifariki na kufikisha jumla ya vifo vya watumishi watano katika ajali hiyo.
Watumishi waliopoteza maisha katika ajali hiyo ni; Ramadhani Gumbo ambaye alikuwa ni Meneja Usafirishaji Kanda ya Tanga, Eng. Fabiola Moshi ambaye alikuwa Meneja Ukarabati wa Mabehewa ya abiria kanda ya Dar es Salaam, Joseph Komba aliyekuwa Meneja Msaidizi Usafirishaji Kanda ya Dar es Salaam, Philibert M. Kajuna; Mtaalamu wa Usalama wa Reli pamoja na George Urio ambaye alikuwa dereva wa Kiberenge
Mpaka sasa aliyejeruhiwa ni mtu mmoja ambaye ni Elizabeth Bona aliyekuwa muongoza treni anaendelea na matibabu.
Jamila ameeleza kuwa uchunguzi wa kujumuisha kwa kushirikiana na taasisi nyingine utafanywa ili kubaini chanzo cha ajali hiyo ambacho mpaka sasa hakijajulikana, na amsema taarifa zaidi zitaendelea kutolewa kuhusu maandalizi ya kuhifadhi miili ya watumishi hao.
Mwisho.