Waziri wa afya nchini Tanzania, Ummy Mwalimu amethibitisha kisa cha kwanza cha mgonjwa mwenye maambukizi ya virusi vya Corona leo Machi 16, 2020 wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Mgonjwa huyo ni mwanamke mwenye umri wa miaka 46 ambaye ni Mtanzania, aliyepokelewa jana nchini Machi 15, 2020 kwenye uwanja wa ndege KIA.
Waziri Ummy amesema baada ya mgonjwa huyo kupimwa jana pindi alipofika KIA hakukutwa na homa lakini baadaye alipofika hotelini alianza kujisikia vibaya na kwenda hospitalini ili kuchukuliwa vipimo ndipo alipogunduliwa tayari ana maambukizi ya virusi vya Corona na kwasasa yupo katika hospitali ya Mount Meru Arusha anaendelea vizuri na matibabu.
Aidha, Waziri Ummy amewatoa hofu Watanzania kwa kusema kuwa serikali imejiandaa kukabiliana na ugonjwa huo na inashirikiana na WHO pamoja na wadau wengine ili kutokomeza ugonjwa huo huku akiwataka wananchi kuchukua tahadhari mapema.
Ametoa wito kwa Watanzania wasiokuwa na safari za lazima nje ya nchi kusitisha safari hizo na pia kuweka vifaa vya kunawia mikono kwa maji tiririka na sabuni pamoja na vitakasa mikono ,kuweka maji yenye dawa ya Chlorine kwa ajili ya kusafisha mikono kwenye maeneo ya mikusanyiko yenye watu kama vile nyumba zakulala wageni, vituo vya mabasi, na kuzitaka hospitali za serikali na binafsi kuwekwa zuio la watu wengi kuruhusiwa kumuona mgonjwa hospitalini.
Mwisho.