Mwenyekiti wa Chama cha Walimu mkoa wa mara CWT Livingston Gamba ameongoza mamia ya waombolezaji katika mazishi ya mwalimu wa shule ya msingi sirari Rose Gulinja aliyekutwa ndani ya gari lake akiwa amenyongwa hadi kufa na watu wasiojulikana.
Taarifa na Jumanne Ntono
Mwalimu Rose Gulinja aliuawa mnamo tarehe moja mwezi wa pili mwaka huu na mwili wake kukutwa umetelekezwa ndani ya gari lake katika eneo la nchi jirani ya Kenya umbali wa mita 200 kutoka mpaka wa Sirari na nchi hiyo.
John Wegesa Heche ambaye ni mbunge wa jimbo la Tarime mjini amekemea kitendo cha mwalimu huyo kuawa na ameliomba jeshi la polisi kufanya uchunguzi wa kina ili wahusika wachukuliwe hatua za kisheria.
Mwenyekiti wa chama cha walimu wilaya ya Tarime shirikisho Nyagosaima amesema jamii inapaswa kutoa ushirikiano ili kuzuia matukio ya walimu wanaofundisha ndani ya mkoa wa Mara kuawa .
Baadhi ya walimu na wanafunzi shule ya msingi Sirari wamelaani mauaji ya mwalimu huyo na kuiomba jamii kuacha kuwaua walimu ili wawasaidie kupata elimu.
Katika tukio hilo la mauaji hayo, mtoto mwenye umri wa miaka 6 Jonathan Bulugu aliyekuwa ndani ya gari na mwalimu huyo alinusurika kufa
Mwisho.