Wizara ya Maliasili na Utalii imetangaza kuanza kutoa vibali rasmi vya kuanzisha mashamba na bucha za Wanyamapori kwa watanzania wenye kipato cha chini ikiwa ni sehemu ya kutekeleza agizo liilotolewa na rais wa Jamhuri ya Muungano Dokta John Magufuli Oktoba 10 mwaka 2019 alipokuwa ziarani Mkoani Katavi.
Taarifa na Beatrice Gerald.
Akizungumza na Wanahabari Mkoani Arusha ,Waziri wa Wizara hiyo Dokta Hamis Kigwangala amesema Wizara hiyo tayari imeanza hatua za awali ikiwemo marekebisho ya sheria pamoja na kushusha ada ya uanzishaji mashamba hayo.
Dokta Kingwangala amesema biashara hiyo itafanyika kwa msimu mzima wa mwaka kwa wafanyabiashara wenye mashamba ya wanyamapori ambao watakuwa wamekidhi vigezo.
Ujio huo wa maduka ya nyamapori inapokelewa kwa hisia tofauti na baadhi ya wakazi mkoani Arusha ambao wamesema kuwa fursa hiyo itakuwa chanzo kingine cha mapato kwa Wizara hiyo ambayo imekuwa ikitegemea shughuli za Utalii.
Uanzishwaji wa maduka hayo ya nyamapori unatajwa kuja kupunguza Uhalifu hasa Ujangili,huku Walengwa wakuu wa ulaji wa Nyama hiyo wakitajwa kuwa ni Watanzania wanaoishi kwa kipato cha Chini.
Mwisho.