Wakazi wa wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro wameeleza kupoteza matumaini ya uwezekano wa kukamilika kwa Barabara ya Lami kutoka Kidatu hadi Ifakara yenye urefu wa KM 66.9 ambayo iliwekewa jiwe la msingi mwanzoni mwa mwezi Mei 2018 na Rais Magufuli, ambapo mpaka sasa utekelezaji wake ni asilimia 10 pekee.
Habari na Omary Hussein.
Mradi huo wa barabara ya kiwango cha Lami kutoka Kidatu-Ifakara yenye urefu wa KM 66.9 ambao utekelezaji wake umepangwa kugharimu kiasi cha Shilingi Bilion 111.4 unaotekelezwa kwa ushirikiano baina ya Tanzania, Jumuiya ya Umoja wa Nchi za Ulaya, Shirika la misaada la Uingereza pamoja na Shirika la misaada la Marekani (USAIDS).
Mnano Mei 04 mwaka 2018 Rais Dkt.John Pombe magufuli pamoja na viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi aliweka jiwe la msingi katika mradi huo, ambao kwa mujibu wa mkataba unapaswa kutekelezwa ndani ya miezi 30.
Barabara hiyo ambayo ni mwaka wa tatu mpaka sasa ambayo wakazi ambao ni watumiaji husika wamekiri kwamba bado hakuna matumanini, kwa kuwa mkandarasi yupo nje ya wakati kwa asilimia 90, na wamebainisha kuwa kusuasua kwa ujenzi wa barabara hiyo unawaongezea machungu hasa unapofika msimu wa mvua.
Aidha, pamoja na wananchi kukiri kuwa mradi uko nyuma ya wakati, watekelezaji wanaohusika na mradi huo wamesema kilicho wachelewesha ni kukwama kwa vitendea kazi bandarini vilivyokuwa vikishikiliwa kwa ajili ya kulipia kodi.
Mradi wa barabara ya Kidatu-Ifakara unatakelezwa na mkandarasi wa Kampuni ya Reynolds Construction kutoka Nigeria, ambao ni mradi wa miaka mitatu na ulipangwa kukamilika Aprili mwaka huu wa 2020 mpaka sasa unasuasua na haujakamilika.
Mwisho.