Polisi mkoa wa Mwanza kwa kushirikiana na vyombo vingine vya kiusalama wamewakamata watu saba waliojifanya ni maofisa wa usalama.
Watu hao wamedakwa wakidaiwa kujifanya maofisa usalama wa nchini Tanzania .
Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza amesema watu hao wanatuhumiwa kuwatapeli wananchi na watumishi wa serikali huku wakiwajengea hofu wakazi wa jiji la Mwanza kwa mbinu ya mazingira ya kupewa rushwa.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 7, 2020, kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro amesema matukio hayo yametokea kati ya Disemba 27, 2019 na Januari 2, 2020 maeneo ya Nyakato wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza.
Muliro amesema watuhumiwa hao walikuwa wakitumia Gari aina ya Toyota la kubeba wagonjwa yenye usajili wa namba T.751 BNL ambalo walisema ni sehemu ya msafara wa viongozi wakuu.
"Walikamatwa na makachero na wakaendelea kujitambulisha kuwa wao ni maofisa usalama wa taifa toka ikulu lakini walipohojiwa kwa kina ilibainika ni matapeli" -Jumanne Muliro-Kamanda wa Polisi Mwanza .
Kamanda Muliro amewataja watuhumiwa hao saba kwa majina na umri kuwa ni: Chalanga Chalanga (45) mkazi wa Pasiansi Mwanza na Arusha, Hamis Mwalimu (25), Philipo Petro (35) mkazi wa Misungwi, Elia Gunda (30) mkazi wa Kisesa, Hassan Juma (29) mkazi wa Mkolani, Selemani Karanga (25) ambaye alijifanya mlinzi wa Chalanga Chalanga na Michael Mazigemkazi mkazi wa Morogoro.
Aidha, kamanda Muliro amesema watuhumiwa tayari wamehojiwa na upelelezi ukikamilika watafikishwa Mahakamani.
Mwisho.