Baadhi ya wafugaji katika mikoa ya Pwani na Morogoro wameiomba serikali kufanya utafiti kubaini Dawa halisi ya kutokomeza wadudu wasumbufu wakiwemo Kupe weupe, wakisema pamoja na wengi wao kujitokeza kuogesha mifugo yao katika majosho yaliyopo lakini bado dawa zilizopo haziwasaidii .
Wafugaji wamesema pamoja na kutambua umuhimu wa kutunza mifugo na kujitahidi kuihudumia kadiri wanavyoweza changamoto inayowasumbua ni dawa wanazotumia ambazo zinawagharimu huku mifugo ikiendelea kudhoofika.
Katika josho la kata ya Vigwaza wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani wafugaji wameamua kufanya uhamasishaji juu ya zoezi la kuogesha mifugo, lakini kilio cha wafugaji hao ni wadudu wasumbufu wakiwemo kupe weupe.
Uhamasishaji huo wa uogeshaji wa mifugo katika majosho unatekelezwa na serikali kupitia wizara ya mifugo, wataalam nao wanasema vifo vyote vya wanyama ukiachana na magonjwa ya mlipuko zaidi ya asilimia 75 husababishwa na Kupe.
Msisitizo kwa wafugaji umetolewa ikiwa ni kutambua, suala la kuogesha mifugo si hiari kwakua ni suala lililoainishwa kisheria ambapo wametakiwa kutumia kamati zao kuainisha changamoto zinazo watatiza zinazowafanya washindwe kutimiza wajibu huo.
“Tunawataka wafugaji kwa kanda hii ya mashariki na wote nchi nzima waone kama ni jukumu la lazima na kisheria kuogesha mifugo yao”.Amesema Joyce Daffa – Kiongozi wa timu ya kanda ya ufuatiliji wa uogeshaji mifugo.
Takwimu za wizara ya Mifugo zinaonyesha kwa nchi zima kuna jumla ya Majosho 1,733 ya serikali yanayofanya kazi, na kupitia kampeni hii, mpango ni kuwawezesha wafugaji kutumia majosho kuogesha mifugo yao kutokomeza magonjwa yanayo epukika.
Mwisho.