Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza ACP Muliro Jumanne amekanusha taarifa zilizokuwa zinasambaa katika mitandao ya kijamii zikieleza kuwa kuna wanachama hao wa CHADEMA wametekwa jijini Mwanza.
Muliro amesema hakuna utekaji uliotokea bali wanachama hao walikamatwa na jeshi la polisi kwa ajili ya mahojiano baada ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema wa mtaa wa Mahina.
Kamanda Muliro, akizungumza na waandishi wa habari amesema baada ya kupatikana taarifa zilizokuwa zibainisha kuwa siku ya Disemba 29, Mwaka huu Majira ya 15:00 mtaa wa Mahina Kata ya Mahina wilayani Nyamagana kulipatikana taarifa toka kwa raia wema kuwa kumeonekana watu wawili waliohisiwa kuwa siyo watu wema wakiwa karibu na Hoteli ya Paradise.
“Jeshi la polisi lilifanya ufuatiliaji wa haraka na kufika eneo hilo na kuwakamata watu hao wawili, ambao katika mahojiano ya awali walikataa kutoa utambulisho wao kuwa wamefika maeneo hayo kufanya shughuli gani”, Amesema ACP Muliro.
Amesema baada ya wanachama hao kukamatwa walichukuliwa na kupelekwa kituo cha polisi cha kati na kutoa ushirikiano kwa askari pia kutaja majina yao kuwa ni Abdukarimu Muro (31), ambaye ni afisa habari wa katibu mkuu CHADEMA Mkazi wa Kinondoni B, Dar es Salaam na Said Haidani (30), Dereva wa katibu mkuu CHADEMA, Mkazi wa Mbezi Kimara Dar es Salaam wameambatana na Katibu Mkuu CHADEMA, Mh. John Mnyika pamoja na polisi waliwaachia huru baada ya kujiridhisha hawakuwa wahalifu.
Jeshi la Polisi mkoa wa Mwanza limetoa onyo kwa watu wasiokuwa na taarifa rasmi na wenye tabia ya kuzusha mambo hasa watu wanapokamatwa kwa kusema wametekwa waache tabia hiyo.
Aidha,amesema hali hiyo yakutoa taharuki ininazusha taharuki kwa jamii na kwa kufanya hivyo ni makosa na hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao pindi watakapobainika.
Mwisho.