Wasomi na wahitimu wa elimu ya juu nchini, wameshauriwa kuwa wabunifu na kuachana na kasumba ya kuchagua kazi za kufanya ili kukabiliana na changamoto ya uhaba wa ajira.
Wahitimu zaidi ya mia nne na tisini wa mafunzo ya ngazi mbalimbali, katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino tawi la Arusha wanategemea kupata ajira kulingana na taaluma walizosomea.
Ni ukweli usio na shaka kuwa, suala la ajira ni mtihani mwingine wa maisha unaowasubiri. Na hii ndiyo sababu wanashauriwa kuwa wabunifu ili kukabiliana na changamoto hiyo.
Profesa Adelardus Kilangi ambaye ni Mwanasheria mkuu wa serikali ya Tanzania, analiona soko la ajira mbele yake, hasa iwapo wahusika watatumia usomi wao na fursa zilizopo nchini.
Ni kutokana na changamoto hiyo na nyinginezo, inaelezwa kuwa soko la ajira haliwezi kuongezeka na badala yake litazidi kupungua mwaka hadi mwaka, kutokana na ongezeko la wahitimu wa vyuo vikuu na kada nyingine.
Mkuu wa wilaya ya Arusha Gabriel Daqaro, amewashauri wasomi kutotumia elimu yao kuhujumu rasirimali za nchi.
Baadhi ya wananchi na wahitimu wameishauri serikali, kutoa mtaji wa fedha au nyenzo za kazi kwa wahitimu wa vyuo wenye nia na mipango madhubuti ya kujiajiri.
Mwisho