Mwanafunzi mmoja Matutu Mashini (7) aliyekuwa anasoma darasa la kwanza katika shule ya msingi Salama A, iliyoko katika wilaya ya Bunda mkoani Mara, amekufa maji, baada ya kutumbukia katika kisima kirefu wakati akichota maji.
Kwa mujibu wa afisa mtendaji wa kijiji cha Salama A, Mashaka Maulilo, tukio hilo limetokea juzi majira ya saa tano na dakika 20 asubuhi kijijini hapo wakati mtoto huyo pamoja na wenzake watatu wakichota maji katika kisima hicho. Maulilo amesema kuwa wakati mtoto huyo akichota maji chombo chake alichokuwa akitumia kuchota maji kilimtoka mkononi na kwenda katika kina kirefu, ambapo alikifuatilia na kuzidiwa na maji hayo na ndipo akapoteza maisha. Aidha, amesema kuwa wenzake walikwenda kutoa taarifa kwao, ambapo yowe ikapigwa na wananchi wakaenda katika eneo la tukio na kuanza kuutafuta mwili wa marehemu kwa kuzamia katika kisima hicho na ndipo wakafanikiwa kuuopoa na kwenda kuuzika. Afisa mtendaji huyo ametoa wito kwa wazazi na walezi kuacha tabia ya kutuma watoto wadogo kwenda kuchota maji kwenye visima, wakati wakiwa hawana mtu mzima, akisema kuwa kama kungekuwa na mtu mzima mtoto huyo uhenda angeokolewa.