Wananchi wa wilaya ya Igunga na Nzega mkoani Tabora wameiunga mkono Kampeni ya Fukuafukua Majambazi na Vibaka kwa kupiga kura za siri kuwataja wahalifu ambao wanasumbua katika maeneo yao iliyoanzishwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa huo.
Kampeni hiyo inaongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa wa Tabora na kuratibiwa na Kamanda wa polisi wa mkoa kwa wananchi kupiga kura za siri katika mikutano ya hadhara na mtu ambaye atatajwa mara nyingi zaidi atafanyiwa uchunguzi wa kina na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria. Baada ya Wananchi kupiga kura za siri kura hizo zilihesabiwa na majina ya wale waliopata kura nyingi za uhalifu yakatajwa hadharani mbele ya Wananchi. Huku Mkuu wa mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akisisitiza msimamo wa Serikali ni kuona Wananchi wake wanakuwa salama wakati wote na kupata fursa ya kufanya shughuli zao za maendeleo bila bugudha yoyote. Kuanzishwa kwa kampeni hiyo Wananchi wameonyesha kufurahishwa na hatua hiyo ya serikali ya mkoa wa Tabora.