Shirika la umeme nchini Tanesco Kanda ya Dar es salaam limefanya ukaguzi wa akaunti za luku eneo la Mchikichini wilaya ya Ilala na kubaini upotevu mkubwa wa umeme kutokana na wizi unaofanywa na baadhi ya wananchi na kusababisha shirika hilo kupata hasara.
Katika zoezi hilo zaidi ya nyumba mia tatu zimekaguliwa na nyumba sita kati ya hizo zimegundulika kutumia umeme bila malipo. Baadhi ya wananchi waliokutwa katika nyumba zilizobainika kufanya wizi wa umeme wamekana kuhusika na wizi huo kwa kueleza kuwa, wamekuwa wakitoa fedha ya umeme kwa wamiliki wa nyumba wakijua umeme unanunuliwa. Mdhibiti Mkuu wa Mapato wa Shirika la umeme nchini Tanesco Kanda ya Dar es salaam na Pwani Mhandisi Mrisho Sangiwa amesema baadhi ya waliowabaini hawajawahi kununua umeme kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitatu licha ya kuitumia nishati hiyo. Aidha Mhandisi Mrisho Sangiwa amesema kwa mujibu wa sheria ya umeme ya mwaka 2008 kuiba umeme ni kosa la jinai kwani ni kuingilia miundombinu ya serikali hivyo hatua ya kwanza ni kusitisha huduma ya umeme kwa waliobainika na watuhumiwa hao kuwa na kesi ya kujibu kwa kuvunja sheria.