Vijana wawili wa Kitanzania, Zakaria Sheha Ally na Shamsi Mwalimu Said wamechukua nafasi ya kwanza na ya tatu kwenye fainali za 27 za tuzo ya kimataifa ya kuhifadhi Quran tukufu. Zakaria Sheha Ally (16) kutoka Tanzania Bara na Shamsi Mwalimu Said (19) kutoka Zanzibar wameibuka na kitita cha dola za Marekani 5,000 na dola 3,000 kila mmoja baada ya kuwashinda wenzao nane waliofanikiwa kuingia fainali hizo ambao walitoka Afrika Kusini, Sudan, Malaysia, Uturuki, Yemen, Kenya, Burundi na Uingereza.
Nafasi ya pili imechukuliwa na kijana Gaffari Mohammed (14) kutoka Uingereza ambaye ameibuka na kitita cha dola za Marekani 4,000. Mashindano hayo yaliyoandaliwa na Jumuiya ya Kuhifadhisha Quran Tanzania, mwaka huu yalishirikisha vijana 10 kutoka nchi 10 duniani.
Tuzo hizo zimetolewa wakati wa kilele cha mashindano ya 27 ya Kimataifa ya Kuhifadhi na Kusoma Qur’an tukufu na utoaji tuzo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na mamia ya waumini wa Kiislamu waliofurika kushuhudia kilele cha Tuzo ya Kimataifa ya Quran iliyoandaliwa na Jumuiya ya Kuhifadhisha Quran nchini, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuhifadhisha Quran kunapaswa kuwa msingi imara katika kujenga jamii bora.
“Tuendelee kuhimiza suala la malezi bora ya vijana wetu kwa lengo la kuwafanya wawe raia wema, wakweli, wazalendo na wenye manufaa kwa nchi yao. Quran inatusisitizia sana kuhusu suala la uadilifu. Kwa mfano, katika Quran 9:119, Mwenyezi Mungu Mtukufu anatukumbusha waumini kumuogopa Mungu na kuambatana na wale walio wakweli wa maneno na vitendo,” amesema Waziri Mkuu.