Wizara ya Maji na Umwagiliaji imetenga zaidi ya shilingi milioni 700 kujenga miundombinu ya maji katika mji wa Mirerani wilayani Simanjiro mkoani Manyara ikiwa ni utekelezaji wa ahadi ya Rais John Magufuli aliyoitoa wakati wa uzinduzi wa barabara ya KIA –Mirerani Septemba mwaka huu.
Mwezi uliopita Rais Magufuli alizindua barabara ya KIA-Mirerani ambapo katika uzinduzi huo aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Manyara dkt Joel Bendera alitoa kilio cha wakazi wa mji wa Mirerani kuwa ni maji. Ahadi ya Rais Magufuli imeanza kutekelezwa na Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kutenga zaidi ya shilingi milioni 700 zinazohitajika kuchimba visima.
Akiongea katika ziara ya kukagua miundo mbinu ya maji katika mji wa Mirerani, Waziri wa Maji na Umwagiliaji Isack Kamwele ameiagiza Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira wilayani Babati BAWASA kusimamia mradi huo ili umalizike kwa muda uliopangwa.
Mkuu wa wilaya ya Simanjiro Mhandisi Zafania Chaula ameipongeza wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kutekeleza kwa wakati ahadi ya Rais Wakazi wa mji wa Mirerani wanasema kupatiwa mradi wa maji itawaondolea kero hiyo iliyokuwa ikiwasababishia matatizo mbalimbali. Waziri Kamwele mbali na kutembela miundo mbinu ya maji katika mji wa Mirerani wilayani Simanjiro pia amekagua mradi wa maji unaojengwa katika mji wa Orkesmeti wilayani humo.