Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Wilison Charles(41)mkazi wa Kijiji cha Kharumwa wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita amefariki Dunia na wengine watatu kujeruhiwa baada ya kuangukiwa na kifusi cha Udongo katika mgodi usio rasmi uliopo kijiji cha Mwasabuka.
Waliojeruhiwa katika ajali hiyo ni Sanda Omari,Emmanuel Makoye na Jumanne Julias na kwamba Wilison Charles ambaye alikuwa na hali mbaya alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika Zahanati ya kijiji cha Kakola wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga mara baada ya kuokolewa.
Kwa Mujibu wa afisa Mtendaji wa Kijiji cha Mwasabuka Adam Elisha ni kwamba Tukio hilo limetokea saa 11jioni Aprili 12,mwaka huu wakati watu hao wakiendelea na shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu kwenye duara namba 270 ambalo liliporomoka na kuwandamiza.
Hata hivyo,Ofisi ya Mgodi wa Mwasabuka chini ya Katibu wa Idara ya Ukaguzi Sijaona Peter imekana kutokeo kwa kifo cha mchimbaji huyo.
Mkaguzi mkuu wa Mgodi huo Bw.Mrefu Malale amesema ukiondoa idara hiyo ya Ukaguzi hata viongozi wengine wa mgodi huo hawana taarifa kwa sababu hakina kifo kilichoripotiwa kwao.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita Kamishina Mwandamizi Msaidizi wa Polisi ASCP Mponjoli Mwabulambo amethibitisha kutokea kwa tukio hilo.
Tukio hilo ni la pili kutokea katika kipindi kisichozidi miezi sita likifuatiwa na tukio lililotokea Disemba 6,mwaka jana ambapo watu Tisa waliangukiwa na kifusi cha Udongo katika mgodi huo na watu saba kati yao walifariki dunia.