Waziri Mkuu Kassimu Majaliwa amezindua soko kuu la Madini ya Dhahabu Mkoa wa Geita,huku akisisitiza watumishi wa serikali wakiwemo wa sekta ya madini kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa kuhakikisha wanaondoa vikwazo vinavyoweza kujitokeza katika uendeshaji wa soko hilo.
Amesema kuanzishwa kwa soko hilo kutasaidia kuepusha utoroshaji wa madini hapa nchini pamoja na serikali kukusanya mapato yake kwa uhakika.
Katibu Mkuu Wizara ya Madini Profesa Simon Msanjila amesema makusanyo ya kodi zitokanazo na dhahabu kwa wachimbaji wadogo katika mkoa wa Geita yamepanda kutoka Sh.Bilioni 24 mwaka 2012 hadi kufikia Sh.Bilion 114.78 kwa mwaka 2017/18.
Awali Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel amesema hatua ya kuanzishwa kwa soko hilo ni kutokana na uchumi wa wananchi wa mkoa wa huo kutegemea zaidi shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu kama sehemu ya kujipatia kipato.
Nao wachimbaji wadogo akiwemo Philipo Paulo,Kassimu Iddi pamoja na Mwananyanzala Husein Makubi wamepongeza hatua hiyo ya serikali kwani itasaidia kufanya biashara kwa uhuru zaidi bila vikwazo vilivyokuwa vikijitokeza awali wakati wa usafirishaji wa madini kwenda kutafuta soko la kuuzia.