Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko ametaka ukusanyaji wa mapato katika sekta ya madini ufanyike kwa uwazi bila kificho na kuagiza kuwa kuanzia sasa kazi za kukusanya Maduhuli zinazofanywa na Ofisi ya Madini hazitafanywa na ofisi hiyo pekee bali watashirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama katika eneo husika.
Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko amezungumza hayo mara baada ya kuwasili katika ziara yake ya siku moja Mkoani Geita. Ameeleza kuwa Mikoa ambayo uchumi wake unategemea zaidi madini bado maeneo hayo hayajaonesha matokeo yanayotarajiwa lakini pia kumekua na changamoto ya baadhi ya maeneo kuchimbwa dhahabu lakini sekta husika haina taarifa.
Takwimu za ukusanyaji wa maduhuli kwa mwaka 2010/2011 hadi mwaka 2016/2017 inaonyesha ni jumla ya zaidi ya bilioni 56.
Imeelezwa pia ukosefu wa tafiti za kitaalamu kwa wachimbaji ni tatizo hali inayowafanya wabahatishe katika upatikanaji wa dhahabu. Pamoja na hayo Naibu Waziri Doto Biteko ametembele Mgodi wa Buntubili ambao siku za karibuni mchimbaji mmoja aliangukiwa na kifusi na kufariki na kutaka Wamiliki wote wa migodi wazingatie usalama lakini pia ukaguzi wa mara kwa mara ufanyike migodini.
Picha na mtandao.