Watu wawili wamefariki Dunia na wengine ambao idadi kamili bado haijafahamika wamejeruhiwa baada ya kuibuka vurugu kati ya Askari Polisi na wakazi wa Kijiji cha Ikwambi kata ya Mofu wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro.
Kwa mujibu wa Mkuu wa mkoa wa Morogoro Fatma Mwasa amesema chanzo ni wakulima ambao ni wakazi wa kijiji hicho kuwafungia ndani ya ofisi ya Kijiji wenyeviti wa vitongoji, vijiji pamoja na Wafugaji kwa lengo la kutaka kuwachoma Moto wakiwatuhumu kushindwa kuwasaidia pindi wafugaji wanapoingiza mifugo katika mashamba yao.
Aidha watu wawili hao waliofariki ni Wakulima (mwanamke na mwanaume).
Miongoni mwa waliojeruhiwa ni Diwani wa kata hiyo Greyson Mgonela, ambaye baada ya kufanya mazungumzo naye kwa njia ya simu amesema wakati vurugu zinatokea wananchi walikuwa wakitumia silaha za jadi, Mawe, Mikuki na Marungu kuwapiga Askari, huku Askari nao wakitumia Mabomu ya Machozi na Kisha Risasi za Moto.