Mafunzo ya Kuendeleza Ujuzi yanayotolewa kupitia ruzuku ya Mfuko wa Kuendeleza Ujuzi (SDF) unaoratibiwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) yametengeneza fursa za ajira kwa mamia ya vijana na akinamama katika wilaya ya Rungwe, mkoani Mbeya kupitia mradi wa kufuga samaki.
Mkurugenzi wa shamba la kufugia samaki la RiversBanks Fish Farms Pius Nyambacha ambalo ni miongoni mwa taasisi zilizofadhiliwa na SDF amebainisha hayo alipozungumza na ujumbe kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mamlaka ya Elimu Tanzania (TE) na wawakilishi wa Benki ya Dunia (WB) ambao ni wafadhili wa Mradi huo wa Kuendeleza Ujuzi (SDF).
Amesema ruzuku ya SDF imemwezesha kufuga samaki kitaalam ikiwa ni pamoja na kumpa uwezo wa kuzalisha vifaranga hivyo kumwongezea uzalishaji ambapo katika kipindi cha miezi tisa amezalisha kilo 600 za samaki na hivyo kujiongezea kipato.
Kupitia ruzuku ya SDF, Kampuni ya RiversBanks Fish Farms ilipata ufadhili wa Shil. Milioni 131.2 ambazo zimewezesha kuboresha miundombinu ya uzalishaji vifaranga vya samaki, ufugaji wa kisasa, ununuzi wa vifaa vya kisasa vya ufugaji pamoja na kuendesha mafunzo kwa vijana na wanawake.
Ujumbe kutoka Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia, TEA na Benki ya Dunia (WB) uko mkoani Mbeya kwa ziara ya siku nne ya ukaguzi wa miradi katika taasisi zilizonufaika na ufadhili wa SDF.