Miili ya waandishi wa habari watano pamoja na dereva wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Mwanza waliofariki katika ajali ya gari Januari 11 imeagwa leo Januri 12, 2022 katika uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza.
Viongozi mbalimbali wa dini na serikali akiwemo Waziri wa Habari Nape Nnauye, Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Amina Makilagi ni miongoni mwa wawalioshiriki katika zoezi hilo pamoja na wananchi.
Aidha kwa upande wake Wazir wa Habari Nape Nnauye ametoa siku saba kwa waajiri wanaodaiwa na waandishi wa habari waliofariki katika ajali ya gari wilayani Busega kuhakikisha wanalipa stahiki zao.
"Nimepewa salamu hapa kuwa miongoni mwa waliolala kwenye majeneza hapa mbele yangu kuna stahiki zao hawajalipwa, natoa siku saba kwa waajiri wote wanaodaiwa kulipa stahiki zote za marehemu na kutoa taarifa ofisi ya mkuu wa mkoa"- Alisema Waziri Nape
Nape amesema kuwa waajiri wanapaswa kukumbuka yeye ndiye mwenye leseni za vyombo vya habari hivyo wahakikishe wanakamilisha zoezi loa kulipa stahizi za wwanaodai.
"Yawezekana kuna hali ngumu ya kiuchumi, lakini nasema stahiki zote za marehemu hawa zilipwe ndani ya siku saba. Hayo ya hali ngumu tutayazungumza huko mbeleni kwa waandishi ambao wako hai ila kwa hawa marehemu lazima walipwe"-Aliagiza Waziri Nape
Idadi ya vifo vilivyotokana na ajali hiyo vimefikia 15 baada ya majeruhi mmoja aliyekuwa amelazwa katika hospitali ya rufaa ya Kanda ya Bugando kufariki dunia wakati akipatiwa matibabu.
Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando, Dkt. Fabian Massaga amesema hospitali hiyo ilipokea majeruhi sita wa ajali hiyo ambapo mmoja amefariki na wanne wanaendelea na matibabu huku mmoja akiwa ameruhusiwa kutoka hospitalini.