Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Innocent Bashungwa ameeleza kuwa ataendelea kusimamia upatikanaji wa miundombinu ya michezo kwenye halmashauri na uhai wa michezo ya UMITASHUMTA na UMISETA mashuleni.
Akizungumza wakati wa kukabidhi Ofisi katika Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Waziri Bashungwa amesema kuwa mambo ambayo walikuwa wakiyasimamia na kuyawekea mikakati yanahitaji ushirikiano wa Wizara mbili kama kuhitaji miundombinu katika halmashauri na kurudisha uhai wa UMISETA na UMITASHUMITA vyote kwa pamoja ambayo vipo chini ya halmashauri ambayo inasimamiwa na TAMISEMI.
Waziri Bashungwa alisema katika kipindi cha mwaka mmoja aliokaa alishirikiana vyema na Naibu Waziri na Katibu Mkuu kuhakikisha Wizara hiyo inaamka kutoka kuwa ya ofisini na kuchangamsha sekta za sanaa, utamaduni na michezo kwa matukio mbalimbali ya kiserikali na kushirikiana na sekta binafsi.
“Hii ni wizara muhimu na ya kimkakati inayosimamia Sekta zinazoajiri vijana wengi, kuburudisha na zinazochangia kwenye pato la Taifa,” alisema Waziri Bashungwa.