Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene amesema Rais Samia Suluhu Hassan ametoa msamaha kwa wafungwa wa Tanzania Bara 5704.
Waziri Simbachawene amebainisha hayo leo wakati akizungumza na vyombo vya habari jijini Dar es Salaam ambapo amesema msamaha huo umetolewa kwa masharti kadhaa ikiwemo: "wafungwa wote wapunguziwe robo ya adhabu zao baada ya punguzo la kawaida la moja ya tatu, wafungwa wenye magonjwa ya kudumu ambao hawana uwezo wa kufanya kazi na ugonjwa huo uwe umethibitishwa na mganga mkuu wa mkoa au wilaya, wafungwa wazee wenye miaka 70 au zaidi na wafungwa wote wa kike walioingia na mimba gerezani na wenye watoto wanaonyonya na wasionyonya pamoja na wenye ulemavu..."-Waziri Simbachawene.
Simbachawene amesema ni kwa mara ya kwanza Rais amewaachia wafungwa wenye umri mkubwa na wanaoumwa kwa muda mrefu.
Ametoa rai kwa wafungwa watakaoachiwa kuhakikisha wanajutia makosa yao na kuhakisha wanatumia mafunzo waliyoyapata pindi wa kiwa gerezani kwakuwa serikali haitasita kuwarudisha gerezani ikiwa watapatikana na makosa ya jinai.
Amesema kuwa serikali inashirikiana na wadau wa maendeleo kuwasaidia wafungwa wanaochiwa ili waweze kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa taifa.
Aidha waziri Simbachawene amemtaka kamanda wa polisi kanda maalumu ya Dar es Salaam kumtafuta Mtume na Nabii Josephat Mwingira ili kumhoji juu ya tuhuma mbalimbali alizozitoa.
Hatua hiyo ya Waziri Simbachawene imefuatia baada ya kuwepo kwa taarifa mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii zikimnukuu Askofu Mwingira akitoa tuhuma mbalimbali ikiwemo kutishiwa maisha na mali zake kuteketezwa shambani kwake.
Askofu Mwingira amekaririwa akizungumza hayo kanisani kwake wakati wa ibada Jumapili Desemba 26, ambapo alieleza madhila aliyopitia kutoka kwa serikali.