Serikali imesema inatekeleza mradi wa ujenzi wa majengo mapya ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ambapo tayari imeshatoa shilingi Bilioni 5.9 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo kubwa la ghorofa tatu.
Jengo hilo litatoa huduma za maabara, upasuaji na wodi za kulaza wagonjwa mbalimbali na ili kukamilisha majengo yote zinahitajika jumla ya shilingi Bilioni 13.5, lengo likiwa ni kuimarisha miundombinu ya matibabu ya huduma za kibingwa.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amebainisha hayo katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya jamii ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya Afya na kukagua utoaji huduma kwa wananchi mkoani Singida.
Serikali pia inatekeleza miradi ya maendeleo na mapambano dhidi ya UVIKO-19 ambapo kwa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Singida zimetengwa jumla ya shilingi Bilioni 5.8 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la huduma kwa wagonjwa wa dharura na mahututi, pamoja na vifaa vyake.
Mkuu wa Wilaya ya Singida Pasacas Muragiri akimuwakilisha Mkuu wa mkoa amemhakikishia Waziri wa Afya Dkt. Gwajima kwamba wilaya na mkoa huo imejipanga kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo kwa lengo la kutoa huduma bora kwa wakazi wake.
Wakati huohuo Dkt. Gwajima ametembelea hospitali Teule ya Makiungu iliyojengwa mwaka 1954 na wamisionari ambao walikabidhi hospitali hiyo kwa masista wa kanisa katoliki kwa lengo la kutoa huduma ya afya kwa wakina mama sajawazito wakati wa kujifungua ili kulinda usalama wa maisha ya mama na mtoto.