Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa ameipongeza Jumuiya ya Kihindu nchini kutokana na mchango mkubwa inaoutoa kwenye jamii hususan katika utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya, elimu, maji, michezo na huduma za kiroho ambazo zimekuwa chachu kwa mshikamano na umoja.
Majaliwa amesema sambamba na suala hilo la kiroho, pia Serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na Shree Hindu Mandal kwa upande wa huduma za afya.
“Jambo lililonivutia zaidi kwenye eneo hilo ni Kitendo cha Hospitali zenu kupokea wagonjwa ambao asilimia 95 wanatumia bima ya afya ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).”-Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana usiku (Jumapili, Novemba 14, 2021) wakati alipomuwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya siku ya Diwali inayoashiria kuanza kwa mwaka mpya wa Kihindu 2078 (Vikram Samvat 2078) yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Patel Samaj, Kisutu mkoani Dar es Salaam.
“Kama mnavyofahamu, Serikali ina lengo la kuongeza wigo wa matumizi ya bima ya afya kupitia Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote. Hatua za awali kuhusu Mpango huo zimekamilika na katika bajeti ya Serikali mwaka wa fedha 2022/2023, Rais Samia ameruhusu kutenga jumla ya shilingi bilioni 149.7 kwa ajili ya mpango huo”.
Pia, Waziri Mkuu ameihakikishia Jumuiya ya Kihindu Tanzania kuwa Serikali inaendelea kuheshimu uhuru wa kuabudu kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania na itaendelea kushirikiana nao pamoja na taasisi nyingine za kidini kwa ajili ya ustawi wa Taifa na watu wake.