Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Mwinyi amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Ashatu Kachambwa Kijaji aliyefika Ikulu, Zanzibar kujitambulisha rasmi.
Rais amempongeza Waziri Dkt. Kijaji kwa kuendeleza ushirikiano kati ya Wizara hiyo na Wizara ya Ujenzi na Mawasiliano ya Zanzibar, Ambapo ametaka uhusiano uendelee kuwa imara mara zote kwa maslahi mapana ya taifa.
Aidha Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza haja ya kuendelezwa ushirikiano kati ya Wizara mbili hizo na kusema ana matumaini makubwa mafanikio zaidi yataendelea kupatikana kwa azma ile ile ya kuiletea maendeleo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa upande wake Waziri Dkt. Ashatu Kijaji aliyeongozana na ujumbe wa Wizara yake akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Zainab Chaula amemshukuru Rais Mwinyi na kuahidi kufanyia kazi maelekezo na ushauri alioutoa kwa maslahi mapana ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.