Waziri Mkuu Kaasim Majaliwa ametoa siku saba za awali kwa tume aliyoiunda kuchunguza chanzo cha moto katika soko la kimataifa la Kariakoo uliokuwa ukiteketeza soko hilo kuanzia majira ya usiku wa Julai 10,2021, Ambapo ameitaka tume hiyo kubaini ni nini kimesababisha au nani kasababisha moto huo.
Waziri Majaliwa ametoa kauli leo Jumapili Julai 11, 2021 alipokuwa anaongea na wafanyabiashara na wakazi wa eneo la Kariakoo baada ya kukagua hatua zinazoendela kuchukuliwa kudhibiti moto huo, Jijini Dar es Salaam.
Amesema kuwa kamati iliyoundwa ambayo itafanya kazi na kamati ya ulinzi na usalama iliyoanza kufanya kazi chini ya Mkuu wa Mkoa huo itajumuisha Ofisi ya Rais-Ikulu, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo itawakilishwa na Mkurugenzi wa Maafa.
Wengine ni Vyombo vya Ulinzi na Usalama ikujumuisha Jeshi la Wananchi, Jeshi la Polisi, Zimamoto pamoja na Taasisi ya Kupambana na Rushwa. Pia Waziri Mkuu alizitaja Wakala wa Majengo, Shirika la Umeme (TANESCO), Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).
“ Endapo itagundulika kama kuna mtu alihusika kwa namna moja au nyingine, hatua kali za kisheria zitachukuliwa moja kwa moja, kitendo cha kuungua kwa soko hili la miaka chungu mzima lazima kuwe na uchunguzi wa kina, kwanini leo lishike moto”-waziri Majaliwa.
Aidha, Waziri Mkuu amewataka wafanyabiashara katika soko hilo wawe watulivu wakati Serikali inafanya kazi yake ya kujua chanzo cha moto huo na amewahakikishia usalama wa mali zilizo ndani ya soko hilo.
Waziri Mkuu pia aliwataka wafanyabiashara kutoingia ndani ya soko hilo katika kipindi hiki ambacho udhibiti unaendelea hadi pale timu zilizoundwa zitakapojiridhisha na utulivu na kufanya sensa ya watu wenye mali kuingia mmoja baada ya mwingine ili wakatoe vitu walivyoviacha
“Tunachoshukuru kule chini shimoni hakuna moto, mali zote zinalindwa, msiwe na mashaka milango yote imefungwa na makamanda wako ndani na nje wanalinda, mali zote zimehifadhiwa, msiwe na mashaka”-Amesema Waziri Mkuu Majaliwa.
Kadhalika Waziri Mkuu amewaahidi wafanyabiashara hao kuwa Serikali itaongea na Mabenki yaliyowakopesha wafanyabiashara waliounguliwa na mali zao kuwaongezea muda wa kulipa mikopo yao baada ya kuunguliwa.