Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema sasa umefika wakati wa kuangalia kwa undani vikwazo vilivyosababisha vijana kutokuwa na jukwaa la pamoja ambapo amesema ni muhimu kuanzishwa kwa baraza la vijana litakalowezesha kuweka ajenda zao kitaifa.
Rais Samia amebainisha hilo leo Juni 15, ikiwa ni siku ya tatu ya ziara yake Mkoani Mwanza, Ambapo amesema kipindi hiki ni cha vijana kusimamia maendeleo ya nchi.
Amewataka vijana wanaopata fursa mbalimbali nchini kuzitumia vema kwa kulitumikia Taifa kwa umakini na ufanisi, “Sisi viongozi wenu kazi yetu kuonesha njia vijana wapite na muendelee na safari ya maendeleo lakini pia kulilinda na kuendeleza Taifa hili”-Rais Samia.
Rais Samia amesema hata Baraza la mawaziri wengi ni vijana sambamba na wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa walioteuliwa wengi wao ni vijana.
“Mfano mzuri kule Zanzibar, Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Mwinyi ni kijana na tulimpendekeza tukijua hii ni enzi ya vijana, kwa hiyo vijana tunaomba mjitambue kwamba nyinyi sasa ndio wenye maono ya nchi hii sasa hivi na baadaye na mwelekeo ni huo".
Aidha, Rais Samia pia amesema atafanya mabadiliko ya wakuu wa wilaya hivi karibuni na atawapa nafasi zaidi vijana.
“Kuna mkeka wa Ma-DC (wakuu wa wilaya) utakaotoka hivi karibuni..., ninataka kuwaambia wote ni vijana. Kwa hiyo hizo ndizo fursa mlizonazo vijana ingawa baadhi yenu tunavyowapa fursa hizi mnakwenda kufanya mnayofanya na mnatuangusha”-Amesema Rais Samia.
Kupitia kauli yake hiyo Rais amewafuta kazi mkuu wa Wilaya ya Morogoro na mkurugenzi wa halmashauri hiyo baada ya kuchukizwa na jinsi walivyoshughulikia suala la wafanyabiashara wadogo wilayani humo.
Rais Samia amemwagiza Waziri wa Tamisemi, Ummy Mwalimu kutekeleza agizo lake la kutengua uteuzi wa viongozi hao.
"Kutokana na kutengewa eneo lililo nje lisilofikiwa na wateja, wamachinga Morogoro waliamua kurejea mjini na mamlaka ikaingilia kati kuwaondoa. Sijafurahia jinsi walivyotendewa na DC na mkurugenzi hawana kazi. Kwa sababu kuna njia nzuri zaidi ambayo ingetumika kushughulikia hilo..., sio ile iliyotumika. Sijafurahishwa nakuagiza Waziri wa Tamisemi shughulikia hilo".
Tamati ya ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan imekamilika kwa yeye kushiriki hafla ya utiaji saini mikataba mitano ya ujenzi na ukarabati wa Meli pamoja na uzinduzi wa meli za Mv. Viktoria na Mv. Butiama ambazo awali zilifanyiwa ukarabati na chelezo.