Rais Mstaafu wa Tanzania wa awamu ya pili Dkt. Ali Hassan Mwinyi amemtembelea Rais Samia Suluhu Hassan nyumbani kwake leo Aprili 12, na kufanya naye mazungumzo.
Rais mwinyi amempongeza Rais Samia kwa namna alivyoanza utendaji wake wa kazi na kusema kuwa ameanza vizuri majukumu yake ya kuliongoza taifa hili la Tanzania.
Mwinyi amesema lengo lake la kufanya ziara hiyonyumbani kwa Rais Samia lilikuwa kumjulia hali rais Samia na kumhakikishia msaada wowote atakaohitaji katika majukumu yake kama kingozi wa Tanzania.
"Mama ameanza vizuri, ingekuwa ni nyimbo ningesema once more!!!, ameanza vizuri kabisa na kila mmoja ana furaha, kila Raia unayemsikia anasema Mama ameanza vizuri, tuliyekuwa nae tulikuwa na Rais mzuri sana, mzoefu wa mambo ya kiserikali, ametufanyia kazi nzuri sana, sasa kaacha mambo haya ghafla kamwachia mwenzie. Mama naye ni Mwanadamu atakuwa na yake na vilevile kuna mambo ambayo yameanzwa na Mtu mwingine ambayo Watu wanayataka wanayapenda, wanamshikilia Mama tunayataka haya tunayataka! tulieni tutayatekeleza haya sasa hilo linafurahisha"-Rais Mstaafu Mwinyi.
Aidha, Rais Mstaafu Mwinyi ametoa rai kwa Watanzania kumuunga mkono rais Samia Suluhu Hassan na kuepuka tofauti ambazo zitalirudisha nyuma taifa, na pia amesisitiza kufanya kazi kwa juhudi pamoja na kuwa na mshkamano.