Mamia ya wazanzibari wanaendelea kumiminika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja vilivyopo mjini Ujunga ambapo ndipo mwili wa aliyekuwa makamo wa kwanza wa Urais Zanzibar utakapopelekwa kwa ajili ya dua kabla ya kusafirishwa kijijini kwake Mtambwe, kisiwani Pemba.
Kifo cha Maalim Seif Sharif Hamad kinaonekana kuleta simanzi kubwa kwa wakazi wa visiwani humo na watanzania kwa ujumla.
Kisiwani Pemba ambapo ndio alikuwa ngome yake Kuu wakati wa uhai wake, punde tu baada ya taarifa za kifo chake kuenea, baadhi ya maduka yamefungwa na shughuli nyingi za mji kusimama, hivyo kufanya mji huo kuzizima kwa saa kadhaa.
Ratiba ya mazishi inaonyesha kuwa, baada ya mwili wa marehemu utaswaliwa katika viwanja vya Mnazi Mmoja na hatimaye kwenda kupumzishwa huko kijijini kwao Mtambwe.
Wakati maombolezo yakiendelea, wafanyakazi wa Shirika la Msalaba Mwekundu wameonekana wakiwanyunyizia watu sanitaiza huku wachache Wakionekana kuchukua tahadhari ya kuvaa barakoa.
Mpaka kifo chake, Maalim alikuwa makamo wa kwanza wa urais Zanzibar chini ya serikali ya umoja wa kitaifa.
Maalim anazikwa wakati watanzania wapo katika kuomboleza msiba mwengine wa aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi aliyefariki jana Februari 17, majira ya saa tatu usiku.
Chanzo na BBC Swahili.