Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na mbunge wa kuteuliwa Humphrey Polepole amesema kuwa Rais wa Tanzania John Magufuli hana mpango wa kuongeza muda wa kukaa madarakani.
Akijibu swali la Mbunge wa Konde, Khatib Said Haji kupitia chama cha ACT-Wazalendo bungeni leo, Polepole amesema kuwa Rais hataongeza muda wowote.
“Masuala ya Chama cha mapinduzi hujadiliwa kwenye vikao vya chama , hapa bungeni wabunge wana uhuru wa kuzungumza lakini kinachozungumzwa humu ndani hakiathiri msimamo wa Chama cha Mapinduzi ambao tumeshautoa, Rais hataongeza muda”- amesema Polepole.
Mjadala wa kuongeza muda wa rais madarakani umerejea tena hivi karibuni baada ya wabunge wawili wa Chama Cha Mapinduzi kuchangia Bungeni hoja ya kutaka Rais Magufuli aongezewe muda wa kukaa madarakani.
Awali, katika muhula wa kwanza wa Rais Magufuli alipuuzia mapendekezo hayo kutoka kwa baadhi ya wabunge wa Bunge lililopita akiahidi kuwa hataongeza muda wa kukaa madarakani.