Rais wa Msumbiji Filipe Nyusi amewasili nchini Tanzania leo kwa ziara ya kikazi ya siku mbili.
Nyusi amewasili Wilayani Chato, mkoani Geita na amepokelewa na mwenyeji wake Rais John Pombe Magufuli pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania Prof Palamagamba Kabudi.
Baada ya kufika Chato Rais Nyusi alishiriki katika uwekaji wa jiwe la msingi katika hospitali ya Rufaa Kanda ya Chato ambayo inatarajiwa kuhudumia watu zaidi ya Milioni 18.
Aidha, Mwenyeji wa Rais Nyusi ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amemshukuru Rais huyo wa Msumbiji kufika na kuweka jiwe la msingi katika hospitali hiyo ya kanda ambayo ameahidi itaweza kutoa huduma hata kwa watu wa Msumbiji.
Katika hotuba yake Rais Nyusi amempongeza Rais Magufuli kwa kushughulikia vyema maisha ya Watanzania ikiwa ni pamoja na maendeleo katika nyanja zote kwa ujumla.
“Rais Magufuli anashughulika sana na maisha ya Watanzania, kwa kutafuta maji, chakula, nyumba nzuri za kuishi pamoja na afya… na akiomba afya anataka ile yenye ubora, kwahiyo hii ni zawadi kwetu kutupa nafasi ya kuweka jiwe la msingi”-Rais Nyusi.
Bwana Nyusi aliongeza kuwa “Kule Msumbiji tunameanza mradi wa kujenga hospitali kamili kila wilaya sasa hichi tulichoona hapana ni mfano mzuri kwasababu hii ni hospitali kubwa kuhudumia mikoa mitano au zaidi”-Alisema Rais Filipe Nyusi.
Rais Nyusi ameugusia usalama wa Wanamsumbiji wanaoishi Tanzania pamoja na Watanzania wanaoishi nchini Msumbuji na amesema kuwa kupitia ziara hii ya siku mbili hapa nchini atapata washa wa kuzungumza mambo mbalimbali na Rais Magufuli.
Ziara ya Rais Nyusi ni kwa ajili ya kuendeleza na kuimarisha mahusiano ya baina ya Tanzania na Msumbiji katika maeneo anuwai yakiwemo yale ya kidiplomasia, kiuchumi, kisisasa na kijamii.