Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta John Pombe Magufuli ameitaka Sekretarieti ya maadili ya viongozi kuachana na ujazaji na uwasilishaji wa fomu za maadili ya uongozi kwa njia ya mtandao.
Rais Magufuli amiitaka sekretarieti hiyo kufanya hivyo ili kuepusha uvujaji wa siri na ubadilishaji wa maudhui ya fomu hizo.
Ametoa agizo hilo kwa sekretarieti ya maadili ya viongozi wakati akimuapisha Jaji Sivangilwa Sikalailwa Mwangesi kuwa Kamishna wa Maadili katika hafla fupi iliyofanyika Ikulu Chamwino jijini Dodoma.
Amefafanua kuwa badala ya fomu hizo kujazwa mtandaoni zinapaswa kuchukuliwa mtandaoni na kisha kujazwa na kuwasilishwa nakala halisi kwa ofisi husika.
Aidha, amewasisitiza viongozi wote wa umma wanaotakiwa kujaza fomu hizo za maadili kuhakikisha wanazijaza kabla ya tarehe 30 Desemba, 2020 kwa mujibu wa sheria.
Rais Magufuli amewatakia Watanzania wote heri ya sikukuu ya Krismas na Mwaka Mpya akiwasihi viongozi wasio na zuio la Waziri Mkuu kuruhusiwa kwenda makwao kusherehekea sikukuu na ndugu, jamaa zao.
Baada ya kuapishwa kuwa Kamishna wa Maadili, Jaji Sivangilwa Sikalailwa Mwangesi amemuahidi Rais Magufuli kufanya kazi kwa bidii.
Jaji Mwangesi ameteuliwa kuwa Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili baada ya Jaji wa Mahakama ya Rufani Harold Nsekela kufariki Dunia.