Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini Marekani (FDA) imetoa idhini ya dharura ya matumizi ya maji maji ya damu kuwatibu wagonjwa wa corona.
Mfumo huo wa tiba ambao umeelezwa na wataalam wa afya kuwa unatumia maji hayo kutoka kwa watu waliopona ugonjwa huo, na tayari umewatibu watu zaidi ya 70,000 nchini Marekani.
Rais Donald Trump amesema tiba hiyo huenda ikapunguza idadi ya vifo kwa asilimia 35.
Amesema hayo siku moja baada ya kuishutumu FDA kwa kuweka vizuizi dhidi ya kusambazwa kwa chanjo na tiba zingine kwasababu za kisiasa.
Plasma kutoka kwa wagonjwa waliopona corona ambayo ina antibodies nyingi inaweza kuwatibu wagonjwa wengine, wamesema wataalam wa afya.
"Nimekuwa nikitazamia kufanya hivi kwa muda mrefu, Nafurahia kutoa tangazo la kihistoria katika makabiliano yetu dhidi ya virusi vya China ambavyo itaokoa maisha ya watu wengi-"Rais aliwaambia wanahabari siku ya Jumapili
Mamlaka ya FDA awali ilisema kuwa utafiti umebaini kuwa maji ya damu [plasma] yana uwezo wa kupunguza idadi ya vifo na kuimarisha afya ya mgonjwa ikiwa atafanyiwa tiba hiyo siku tatu za kwanza baada ya kulazwa, japo majaribio zaidi yanahitajika kufanywa ili kuthibitisha uwezo wake.
Shirika hilo lilithibitisha kuwa ni salama kutumia mfumo huo wa tiba baada ya kufanya uchunguzi zaidi data zilizokusanywa miezi ya hivi karibuni, Lakini wataalamu kadhaa, akiwemo Anthony Fauci, mwanachama wa jopo kazi la White House kuhusu coronavirus, wametilia shaka utafiti huo mpaka kufikia sasa.
Katika ujumbe wa Twitter siku ya Jumamosi, rais Trump alisema "Kuna watu, ndani ya FDA ambao wamefanya kuwa vigumu kwa mashirika ya dawa kupata watu wa kufanyiwa majaribio ya chanjo na tiba zingine.
Mapema mwaka huu, Mamlaka hiyo ya udhibiti wa dawa iliidhinisha kwa dharura matumizi ya dawa ya remdesivir kama tiba ya corona.