Wanaume watatu wamekamatwa na polisi nchini Iran kwa kosa la kuwauza watoto wachanga Instagram.
Mkuu wa polisi katika mji mkuu wa Iran -Tehran, Brigadia Jenerali Hossein Rahimi, amesema kuwa mmoja wa watoto hao wachanga alikuwa ni wa siku 20, Mwingine alikua na umri wa mwezi mmoja.
Watoto hao wachanga walikuwa tayari wamenunuliwa kwa hadi dola $500 (£400), na walikua wanauzwa tena kwa dola kati ya $2,000 na $2,500.
Mmoja wa watu waliokamtwa anadaiwa kusema kuwa ''alikuwa anawapata watoto hao wachanga kutoka familia maskini " na "kuwakabidhi familia ambazo zinaweza kuwapatia maisha bora yajayo".
Brigedia Rahimi aliviambia vyombo vya habari vya Tehran kwamba maafisa wa polisi walifahamishwa juu ya "matangazo ya kibiashara katika mtandao wa Instagram yanayouza watoto wachanga".
Maafisa hao waligundua "kurasa 10 hadi 15 za aina hiyo" katika huduma ya kushirikisha picha na kubaini watoto wawili na wanaume watatu waliokua wamekamatwa, alisema. Watoto hao wachanga wamekabidhinwa kwa huduma za kijamii.
Washukiwa walidai kuwa walikuwa wamewaleta watoto kutoka familia maskini kwa "gharama ndogo", kwa mujibu wa Jenerali Hossein.
Katika video iliyochapishwa na Shirika la habari la Young Journalists Club ,mmoja wa wanaume hao alisema kuwa ; "Hii ingewasaidia sana watoto hawa wachanga kuwa na maisha bora yajayo."
Aidha, taarifa zinaeleza kuwa hii sio mara ya kwanza tukio la aina hii kufichuliwa na mamlaka nchini Iran.
Mapema mwaka huu, polisi katika jimbo la Gorgan nchini humo alisema kuwa walikua wamewakamata wanawake wanne na mwanaume mmoja ambao walidaiwa kuwatafuta wanawake maskini wajawazito na kulipia gharama zao za hospitali, halafu wanawachukua watoto wao mara baada ya kujifungua.
Mwaka 2016, aliyekua Makamu wa rais wa masuala ya Familia na Wanawake Shahindokht Molaverdi alielezea wasiwasi wake juu ya kile alichosema kulikua na "idadi ya juu " ya wanawake wanaotarajia kujifungua wanaouza watoto wao wachanga.
Aidha, alisema wanawake wanalazimika kufanya hivyo kwa "sababu mbalimbali", ikiwa ni pamoja na umaskini,uraibu wa mihadarati, ndoa za utotoni na ukosefu wa mahala pa kuishi.