Rais wa Marekani Donald Trump ametangaza kuwa atasaini amri ya kuzuia kwa muda aina zote za uhamiaji nchini Marekani ili kupambana na virusi vya corona.
Katika ujumbe wake wa Twitter ameandika alichokitaja kama "shambulio la adui asiyeonekana ", ambalo ni virusi vya corona pamoja na haja ya kulinda kazi za raia wa Marekani bila kutoa maelezo zaidi.
Haijulikani kufikia sasa ni programu gani za uhamiaji ambazo zitaathirika, huku wakosoaji wake wakisema kuwa Trump anatumia janga la corona kuwafungia milango wahamiaji.
Hii inakuja wakati ikulu ya White House ikisema pia kwamba janga baya zaidi la virusi vya corona limepungua na shughuli zinaweza kuanza kufunguliwa nchini humo.
Marekani ina jumla ya wagonjwa wa corona 782,159 na vifo 41,816 kutokana na virusi hivyo, na tayari imekubaliana na Canada pamoja na Mexico kuongeza zaidi muda wa kuzuia safari zisizo na muhimu baina ya mipaka yao hadi katikati ya mwezi Mei.
Safari pia zimezuiwa kwa kiwango kikubwa kwa watu wanaotoka Ulaya na Uchina kuelekea Marekani, ingawa watu wenye vibali vya kazi vya muda, wanafunzi na wafanyabiashara wanaruhusiwa kuingia.
Tangazo hilo la rais linakuja wakati utawala ukitaka shughuli zifunguliwe katika baadhi ya maeneo ya Marekani ambako zilikuwa zimefungwa kutokana na janga la corona.