Serikali mpya ya Tunisia itakayoongozwa na Waziri Mkuu Elyes Fakhfakh imekula kiapo mbele ya Rais wa nchi hiyo Kais Saied, huku Fakhfakh akiahidi kutatua matatizo ya wananchi wake.
Hafla ya kuapishwa baraza jipya la mawaziri la Tunisia ilifanyika jana baada ya bunge kuidhinisha baraza hilo lililopendekezwa na Waziri Mkuu Fakhfakh.
Bunge la Tunisia liliidhinisha serikali hiyo mpya kwa kura 129 za 'ndiyo' dhidi ya 77 za 'hapana'.
Wakati akiomba ridhaa ya bunge ya kulipitisha baraza la mawaziri alilopendekeza, Fakhfakh aliwaeleza wabunge katika kikao cha siku ya Jumatano cha bunge la nchi hiyo kuwa, atajitahidi kustawisha uchumi na kushughulikia matatizo ya wananchi.
Amesema kustawisha uchumi wa nchi hiyo na kutatua matatizo ya wananchi wa Tunisia ndivyo vitakuwa miongoni mwa vipaumbele muhimu zaidi vitakavyofanyiwa kazi na serikali yake na akawataka wabunge, vyama vya siasa na asasi zote za kiraia nchini humo kuisaidia serikali katika suala hilo.
Hali mbaya ya uchumi hususani tatizo la ukosefu wa ajira ni miongoni mwa matatizo muhimu zaidi yanayoikabili Tunisia kwa sasa, kiasi kwamba katika miaka ya karibuni nchi hiyo imeshuhudia maandamano kadhaa ya kupinga serikali.
Mwisho.