Mfalme Charles wa III wa Uingereza anakwenda Scotland leo kuungana na ndugu, jamaa na waombolezaji wengine ili kuhudhuria ibada ya kumwombea mama yake, Malkia Elizabeth wa II aliyeaga dunia wiki iliyopita.
Hii leo jeneza lenye mwili wa Malkia Elizabeth litapelekwa kwenye kanisa kuu la mtakatifu Giles mjini Edinburgh ambako kutakuwa na ibaada maalum na tukio la kuwasha mishumaa litakalohudhuriwa na familia ya kifalme wakiongozwa na Mfalme Charles. Mwili wa Malkia Elizabeth utalala ndani ya kanisa hilo kabla ya kusafirishwa kwenda mjini London hapo kesho kwa maandalizi ya kuugwa rasmi na kisha mazishi yake kufanyika mnamo Septemba 19. Hapo jana mamia kwa maelfu ya watu walijipanga barabarani kutoa heshima kwa mwili wa Malkia Elizabeth wakati msafara ulioubeba jeneza lake ulipokuwa njiani kutoka kasri la Balmoral kuelekea mji mkuu wa Scotland, Edinburgh.
CHANZO; DW SWAHILI