Watu wanaoishi katika mji wa kaskazini-mashariki wa Kharkiv wameiambia BBC jinsi inavyokuwa ngumu kuishi chini ya mashambulizi ya anga yanayotekelezwa na Urusi.
Glib Mazepas, ambaye anaishi katikati mwa jiji katika mji wa pili wa Ukraine, anasema kumeshuhudiwa "mlipuko mkubwa" usiku kucha kutoka kwa ndege iliyozunguka mara tatu kabla ya kupiga karibu kilomita 1 (maili 0.6) kutoka nyumbani kwake.
Pia alielezea wakati aliposikia shambulio la jana la roketi kwenye Uwanja wa Uhuru wa Kharkiv "Kulikuwa na sauti ya mluzi iliyosikika, kisha mlipuko ukafuata. Nakumbuka nyumba yetu haikuwa ikitetemeka sana kama kutetemeka kutoka kushoto kwenda kulia, kwa takriban sekunde tano. likuwa ni hisia ya ajabu sana."
Mazepas amesema kila kelele anazosikia sasa anafikiri inawezekana ilikuwa ni Urusi imefanya mashambulizi.
"Jana mke wangu alikuwa akipasha moto kitu kwa kutumia ‘microwave’. Na nilishangaa kwa sababu nilifikiri ni aina fulani ya mashambulizi."
Mazepas anasema anashukuru kwa uungwaji mkono wa kimataifa, lakini anataka NATO iende mbali zaidi kwa kutekeleza ukanda wa kutoruka ndege nchini Ukraine.
"Tafadhali funga anga kwa sababu ya makombora ya Kirusi na ndege za kivita za Kirusi. Kwa sababu watapiga tu bomu jiji lote kwenye majivu."