Marekani imewaagiza ndugu wa wafanyakazi wa ubalozi wake nchini Ukraine kuondoka nchini humo huku hali ya wasiwasi ikiendelea kuongezeka katika kanda hiyo.
Wizara ya mambo ya nje pia imetoa ruhusa kwa wahudumu wasio wa lazima kuondoka na kuwataka raia wa Marekani waliopo nchini Ukraine kuangalia uwezekano wa kuondoka.
Katika taarifa yake, imesema kuwa kuna ripoti kuwa Urusi inapanga kuchukua hatua muhimu ya kijeshi dhidi ya Ukraine.
Wizara ya mambo ya nje ya Marekani pia imewaonya watu wasisafiri kwenda Ukraine na Urusi kutokana na hali ya wasi wasi inayoendelea na ''uwezekano wa unyanyasaji dhidi ya raia wa Marekani".
"Kuna taarifa kuwa Urusi inapanga kuchukua hatua muhimu ya kijeshi dhidi ya Ukraine, "lilisema taarifa ya ushauri ya Wizara ya mambo ya nje ya Marekani.
Afisa wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani aliliambia Shirika la habari la AFP kwamba ubalozi unaendelea kuwa wazi lakini akaridia tahadhari kutoka ikulu ya White House kwamba uvamizi unaweza kuja "katika wakati wowote ule'".
Mkuu wa muungano wa ulinzi wa kijeshi wa NATO, ameonya kwamba kuna hatari ya mzozo mpya Ulaya baada ya vikosi vya Urusi vinavyokadiriwa kuwa 100,000 kukusanyika mpakani.
Jumapili, Wizara ya mambo ya nje ya Uingereza ilimshutumu Bw Putin kwa kupanga kumteua kiongozi anayeungwa mkono na Urusi kuiongoza serikali ya Ukraine.