Viongozi wa Umoja wa Ulaya wamerudia ahadi yao ya kushirikiana na nchi washirika za Ulaya Mashariki, wakati ambapo kuna hofu kwamba huenda Urusi ikaivamia kijeshi Ukraine na wameionya Urusi dhidi ya kufanya hivyo.
Hayo yameelezwa jana wakati wa mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya na mataifa ya Ulaya Mashariki ya Ukraine, Moldova, Georgia, Armenia na Azerbaijan. Viongozi hao wameonesha wasiwasi kwamba Urusi inapanga kupeleka majeshi yake karibu na Ukraine.
Viongozi wa Umoja wa Ulaya wametishia kuiwekea vikwazo vikali Urusi, iwapo itaishambulia Ukraine.
Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen amesema wito wao wa kwanza kwa Urusi ni kujiondoa kwenye maeneo ya Ukraine, lakini wamejiandaa pia kwa uchokozi wowote utakaofanywa na Urusi.
''Kama nilivyosema vikwazo vipo, Vikwazo hivyo vinaweza kuimarishwa. Lakini bila shaka kuna vikwazo vilivyotayarishwa ambavyo ni vya ziada na vitawekwa kwenye nyanja zote tofauti".
Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky ambaye ameishutumu Ujerumani kwa kuzuia silaha kuingizwa Ukraine, amesema angependa kuona vikwazo vikali vinawekwa mara moja hata kabla ya vitendo vya kiuchokozi vya Urusi.
Viongozi hao walikutana pembezoni mwa mkutano wa kilele wa Umoja wa Ulaya kutafuta njia ya kuanzisha mazungumzo katika ''Mfumo wa Normandy'' unaowajumuisha viongozi wakuu wa Ukraine, Ufaransa, Urusi na Ujerumani.
Macron na Scholz wanatafuta njia ya kuyafufua mazungumzo na Urusi, huku wakiendelea kuishinikiza Urusi kuzuia kile ambacho nchi za Magharibi zinasema inajiandaa kuishambulia Ukraine.
Baadhi ya nchi za Ulaya zina nia ya kuonesha mshikamano na Ukraine, lakini baadhi zina wasiwasi kuhusu hatua kali za haraka kama vile kuzuia mradi wenye utata wa bomba la gesi unaogharamiwa na Urusi na Ujerumani unaojulikana kama Nord Stream 2, zinaweza zikaichochea Urusi badala ya kuizuia.
#ChanzoDWSwahili