Makundi tisa yanayoipinga serikali ya Ethiopia kikiwemo chama cha Tigray People’s Liberation Front yamekubali kuunda muungano dhidi ya utawala wa Waziri Mkuu Abiy Ahmed.
Hatua ya nakubdi hayo inakuja huku shinikizo likiongezeka kwa Abiy, Ambapo vikosi vya waasi vikipiga hatua kuelekea mji mkuu. Lakini serikali ya Addis Ababa imesema inakaribia kupata ushindi na itaendelea kupigana kile inachokiita kuwa ni vita vilivyopo.
Washirika wa kimataifa wa Ethiopia wametoa wito wa kukomesha uhasama huo.
Mjumbe Maalum wa Marekani katika Upembe wa Afrika yuko Addis Ababa na amefanya mikutano na mawaziri wa serikali.
Msemaji wa Jeshi la Ukombozi la Oromo ambalo ni sehemu ya muungano mpya wa kijeshi na kisiasa aliiambia BBC kuwa lengo lao ni kuondoa serikali ya sasa ya Ethiopia, kuanzisha utawala wa mpito na baadaye kufanya mazungumzo kuainisha mustakabali wa Ethiopia.
Makundi mawili ya waasi wa Oromo na Tigray People’s Liberation Front tayari yameanza kupigana pamoja na wiki hii yalidai kuuteka mji wa Kemise kilomita 325 kaskazini mwa Addis Ababa.
Tangazo rasmi litatolewa Ijumaa asubuhi huko Washington DC Lakini hatua hii inaweza kudhoofisha juhudi za Mjumbe Maalum wa Marekani katika Upembe wa Afrika Jeffrey Feltman ambaye ameanza kukutana na mawaziri wa serikali ya Ethiopia kushinikiza mazungumzo.
Aidha, Pande zote mbili katika mzozo huu zinaendelea kukataa wito wa kusitisha operesheni zao za kijeshi.