Korea Kaskazini imetahadharisha raia wake kusalia majumbani kutokana na hofu ya ''vumbi la njano'' linalopepea kutoka China kuwa linaweza kubeba virusi vya corona.
Mitaa ya mji mkuu Pyongyang iliripotiwa kuwa mitupu siku ya Alhamisi baada ya tahadhari hiyo kutolewa.
Nchi hiyo ambayo imedai kuwa haina maambukizi ya virusi lakini imekuwa kwenye tahadhari kubwa tangu mwezi Januari, huku ikifunga kabisa mipaka na kuzuia mizunguko ya watu.
Televisheni inayodhibitiwa na serikali ya Korea (KCTV) ilitangaza kipengele cha taarifa ya hali ya hewa siku ya Jumatano , ikitahadharisha kuingia kwa vumbi la njano siku inayofuata.
Vumbi la manjano linahusu mchanga kutoka jangwa la Mongolia na China ambalo hupiga Korea ya Kaskazini na Kusini wakati fulani wa mwaka.
Ubalozi wa Urusi huko Pyongyang umesema katika ukurasa wake wa Facebook kuwa wizara ya mambo ya nje ya Korea Kaskazini imeionya pamoja na ofisi nyingine za kidiplomasia na mashirika ya kimataifa nchini humo kuhusu dhoruba ya vumbi ikiwataka wageni wote kubaki nyumbani na kufunga madirisha yao vizuri.
Vyombo vya habari nchi jirani ya Korea Kusini pia vimepinga mawazo hayo na kusema haiwezekani kuwa vumbi la manjano kutoka China linaweza kusambaza ugaonjwa wa Covid-19 kuelekea Korea Kaskazini.
Licha ya kudai kuwa nchi hiyo haina maambukizi ya ugonjwa wa corona, kuna hofu kubwa huko Korea Kaskazini na kiongozi Kim Jong-Un amekuwa akifanya mikutano ya hali ya juu kuhakikisha masharti makali yanatekelezwa.