Kiongozi wa Urusi na mkosoaji mkubwa wa rais wa nchi hiyo Alexeï Navalny, anamtuhumu rais wa Urusi Vladimir Putin kwa kujaribu kumuua kwa sumu.
Kiongozi huyo wa upinzani amethibitisha hilo katika mahojiano na jarida la Ujerumani la Der Spiegel.
Alexeï Navalny alilazwa hospitalini Agosti 20,2020 baada ya kuwa katika hali mbaya huko Omsk, Siberia, na baadaye kusafirishwa siku mbili katika hospitali jijini Berlin, nchini Ujerumani.
Serikali ya Ujerumani ilihitimisha kuwa Navalyn alikuwa amepewa sumu ya Novichok inayoathiri "mishipa ya fahamu', Sumu iliyotengenezwa na jeshi la Kisoviet mnamo miaka ya 1970 na 1980.
Serikali za Magharibi zinataka maelezo zaidi kutoka kwa serikali ya Urusi, ambayo inakanusha kuhusika kwa kitendo hicho na inasema kuwa haina uthibitisho kwamba kitendo hicho ni cha jinai.
Alexeï Navalny aliruhusiwa kuondoka hospitali jijini Berlin wiki moja iliyopita ambako alikuwa akitibiwa.
"Ninathibitisha kwamba Putin anahusika na uhalifu huu na sina maelezo mengine ya kile kilichotokea"-Navalny amesema katika sehemu ya mahojiano yanayotarajiwa kurushwa hewani leo Alhamisi.
Viongozi kutoka kote ulimwenguni walilaani tukio la kupewa sumu kwa kiongozi huyo wa upinzani nchini Urusi Alexei Navalny katika jaribio la kutaka kumuua.